TBA, CRDB KUSHIRIKIANA KATIKA UWEKEZAJI WA SEKTA YA MILIKI

Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kwa kushirikiana na Benki ya CRDB wamefanya kikao cha pamoja kilicholenga kujadili ushirikiano katika uwekezaji wa sekta ya miliki ili kuboresha na kuendeleza makazi nchini.
Kikao hicho kimefanyika Septemba 1, 2025 katika Ofisi za Makao Makuu ya CRDB Jijini Dar es Salaam na kimehudhuriwa na viongozi waandamizi wa pande zote mbili.
Akizungumza baada ya kikao hicho, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Abdulmajid Nsekela, amesema lengo ni kuhakikisha wananchi wananufaika na miradi ya nyumba zinazotekelezwa kwa ushirikiano huo.
“CRDB tuko tayari kushirikiana na TBA. Tunawapongeza kwa mpango huu na tutaendelea kushirikiana ili kuhakikisha wadau wetu wanapata makazi bora na ya kisasa,” amesema Nsekela.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Miliki wa TBA, FRV. Said Mndeme (ndc), amesema kikao hicho kimeweka msingi wa utekelezaji wa miradi mikubwa ya makazi ikiwemo ujenzi wa nyumba za kisasa katika eneo la Canadian Masaki, Jijini Dar es Salaam.
“Tumekuwa na kikao kizuri na uongozi wa CRDB. Tunatarajia kuanza mradi mkubwa wa nyumba za kisasa Masaki na ushirikiano huu utakuwa chachu ya mafanikio katika utekelezaji wake,” amesema Mndeme.
Ushirikiano huo ni sehemu ya utekelezaji wa sera mpya ya Serikali inayotaka TBA kushirikiana na sekta binafsi pamoja na taasisi za kifedha katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.