Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Arch. Daud Kondoro amekutana na Waandishi wa Habari katika ukumbi wa Mikutano wa ofisi ndogo za TBA jijini Dar es Salaam na kutoa taarifa juu gharama na utaratibu wa mauzi ya nyumba za makazi za Magomeni Kota jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika mkutano huo Arch. Kondoro amesema Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameridhia kuwaongezea muda wa manunuzi, wakaazi wa Magomeni Kota kutoka miaka kumi na tano (15) iliyoelekezwa na Serikali awali hadi miaka thelathini (30) ikijumuisha miaka mitano (5) ya kukaa bure.
Arch. Kondoro amesema, nyumba ya chumba kimoja inauzwa shilingi 48,522,913.00 huku muda wa malipo ukiwa miaka 30 na nyumba ya vyumba viwili inauzwa shilingi 56,893,455.00 wakati muda wa malipo ukiwa miaka 30.
Aidha Arch. Kondoro amesema baada ya kuwajulisha kwa barua wakaazi 644, TBA iko tayari kuwatambua wakaazi waliotayari kutekeleza utaratibu huu wa ulipaji na kuingia nao mkataba wa mkaazi mnunuzi. Pia TBA iko tayari kuwatambua wakaazi wasiokuwa tayari kutekeleza utaratibu huu ambao wataruhusiwa kukaa bure kwa miaka mitano (5) na baada ya muda huo kukamilika, nyumba hizo watazirejesha Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) amefafanua Arch. Kondoro.