Leo Desemba 16, 2022 Bodi ya Ushauri ya TBA ikiongozwa na Mwenyekiti wake Arch. Dkt. Ombeni Swai imefanya ziara ya kutembelea na kukagua miradi inayotekelezwa na TBA jijini Dar es Salaam.
Akizungumza mara baada ya kutembelea miradi hiyo Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Arch. Dkt. Swai ameishukuru Serikali ya Awamu sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwa TBA kufanikisha utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa nyumba za makazi kwa watumishi wa Umma ambapo kupitia miradi hiyo itasaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa makazi kwa watumishi wa umma.
Vile vile, Arch. Dkt. Swai ameipongeza TBA kwa kuendelea kutumia Wataalamu wa ndani ambao wametokana na vyuo vilivyopo hapa nchini. Amesema kwa kufanya hivyo TBA inakuza ujuzi na uwezo kwa watalaam hao ambao ni tegemeo kwa taifa.
Pamoja na mambo mengine Arch.Dkt. Swai ameitaka TBA kujiendesha kibiashara ili kuongeza mapato na ushindani katika Soko ambapo amesema kwa kufanya hivyo itaisaidia TBA kujipatia mapato ya kutosha na kufanikisha utekelezaji wa miradi mingi ya ujenzi wa nyumba za makazi katika maeneo mengi nchini.
Bodi hiyo imetembelea miradi mbalimbali ikijumuisha mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi katika eneo la Magomeni na Kijiji Cha Canadian, Masaki jijini Dar es Salaam.