Wafanyakazi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), wametakiwa kubuni
Mikakati mipya yenye ubunifu (innovation) ambayo itawawezesha kutekeleza kwa
ufanisi malengo yao. Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binirith
Satano Mahenge katika Hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya
ya Kongwa Deogratias Ndejembi wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Baraza la
Wafanyakazi wa TBA unaofanyika Dodoma.
“TBA mmepewa dhamana
kubwa ya kutekeleza miradi mikubwa na nyeti yenye sura ya kitaifa na ambayo ina
mchango mkubwa katika ujenzi wa Taifa letu, hivyo mnatakiwa kufanya kazi kwa
kujituma badala ya mazoea ili kufikia malengo”
Aidha Dkt. Mahenge amewataka wafanyakazi hao kutumia Baraza hilo kutazama kwa undani hatua ambazo
TBA imepiga na kujadili maeneo ambayo malengo
ya TBA hayajafikiwa kwa lengo la kuboresha zaidi na kufikia malengo yaliyokusudiwa
na Wakala.
Awali akizungumza katika Mkutano huo Mtendaji Mkuu wa TBA
Arch. Daudi Kondoro amesema TBA imeendelea kutekeleza miradi ya Washitiri
ambayo imegawanyika katika makundi manne (4); Miradi ya Ushauri, Miradi ya
Ujenzi, Miradi ya usanifu na ujenzi na Miradi ya Usimamizi. Hadi kufikia
Desemba, 2019, TBA imetekeleza jumla ya miradi 169.
Baadhi ya Miradi hiyo ni pamoja na Ujenzi wa Radar katika
viwanja vya ndege vya DSM, Songwe, KIA na Mwanza, Ujenzi wa Hospitali ya Rufaa
ya Mkoa wa Geita, Ujenzi wa jengo la Maabara, jengo la upasuaji na mionzi na
jengo la wagonjwa wa nje kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu. Miradi
mingine ni Ujenzi wa Vihenge vya
kuhifadhia nafaka katika Mikoa ya Ruvuma, Njombe, Rukwa, Katavi, Manyara,
Dodoma na Shinyanga pamoja na Mradi wa Ujenzi wa kituo cha pamoja cha Forodha
Kasumulu-Mbeya.
Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Wakala wa Majengo Tanzania hufanyika mara 2 kwa Mwaka kwa lengo la kujadili maendeleo ya Wakala.