KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MIUNDOMBINU YATEMBELEA MRADI WA UJENZI WA NYUMBA ZA MAKAZI MAGOMENI KOTA
Kamati ya Kudumu ya Bunge
ya Miundombinu imefanya ziara kukagua mradi wa ujenzi wa nyumba za Makazi Magomeni
Kota Machi 16, 2020 unaotekelezwa na Wakala wa MajengoTanzania (TBA). Mradi huo
unaotekelezwa na TBA kama Mkandarasi na Mshauri Elekezi, utakapokamilika
unatarajiwa kutoa makazi kwa kaya 644 ambapo mpaka sasa ujenzi wake umekamilika
kwa asilimia 70% na unategemewa kukamilika mwezi Juni, 2020.
Akizungumza mara baada ya kutembelea
mradi huo Mwenyekiti wa Kamati Mhe. Selemani Kakoso (Mb) amesema kuwa kamati
imeridhishwa na kazi inayofanywa katika kutekeleza mradi huu na ameipongeza TBA
kwa ubunifu wa kuanzisha kiwanda cha kuchakata zege na kiwanda cha kufyatulia
matofali kama njia ya kupunguza gharama za utekelezaji wa mradi.
Pia Mhe. Selemani Kakoso
ameiomba Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Ujenzi) kuipa
fedha TBA kiasi cha bilioni 14 ili mradi huu uweze kukamilika kwa wakati. Vilevile,
ameiomba Serikali kuipa TBA vibali vya kuajiri ili kukabiliana na upungufu wa
wataalam 300 uliopo kwa sasa ili kuiongezea ufanisi wa kutekeleza miradi nchini.
Akizungumza katika ziara
hiyo, Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Ujenzi) Mhe.
Elias Kwandikwa (Mb) amesema wataalam kutoka Wizarani watafika Alhamisi ya 19
Machi, 2020 kufanya uhakiki wa gharama zilizotolewa na TBA kujiridhisha na kiasi
cha fedha kinachohitajika kukamilisha utekelezaji wa mradi huo na kuitoa mara
moja pamoja na kuendelea kufuatilia kwa ukaribu mwenendo wa utekelezaji wa
mradi huu.
Akiongea katika ziara hiyo Mtendaji Mkuu wa TBA, Arch. Daud Kondoro amesema TBA imeshaandaa mpango kabambe kwa ajili ya kuendeleza eneo la Magomeni Kota ambapo awamu ya kwanza imehusisha ujenzi wa nyumba za makazi kwa ajili ya kaya 644. Awamu ya pili itahusisha ujenzi wa majengo ya kupangisha pamoja na majengo ya kutolea huduma kwa wakazi watakaokuwa wakiishi katika eneo hili.