Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhe. Prof. Makame Mbarawa (Mb) ametoa pongezi kwa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kwa kukamilisha ujenzi wa Majengo mawili ya makazi katika maeneo ya Magomeni na Msasani Peninsula Masaki yaliyojengwa na TBA kama Mkandarasi na Mshauri Elekezi.
Prof. Mbarawa ametoa pongezi hizo wakati wa Hafla ya Ufunguzi wa Nyumba za Makazi katika Maeneo ya Magomeni Kota na Msasani Peninsula, Masaki zilizojengwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) jijini Dar es Salaam.
Ameongeza kwa kusema kuwa TBA imefanya mapinduzi makubwa ya kiutendaji, kuongeza ubunifu na kujenga majengo mazuri yenye miundombinu ya kisasa kwa lengo la kuongeza mapato zaidi na kuwataka kuongeza miradi mingine mingi kama iliyojengwa Masaki na Magomeni Kota.
Aidha Prof. Mbarawa amesema Majengo yote mawili yamegharimu kiasi cha shilingi Bilioni 10.32 hadi kukamilika kwake na kuwataka wapangaji watakaokuja kuishi katika nyumba hizo kuhakikisha wanazitunza pamoja na kulipa kodi ya pango kwa wakati.
Halikadhalika Prof. Mbarawa ameitaka TBA kuhakikisha inawaondoa wapangaji wote wenye madeni na kuwapatia nyumba Watumishi ambao watalipa kodi kwa wakati.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Selemani Kakoso (Mb) amesema Sekta ya ujenzi ni miongoni mwa vipaumbele muhimu vya Serikali ya Awamu ya Sita ambayo inaendelea kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kama ilivyopangwa. Aidha amesema Bunge litaendelea kuunga mkono ubunifu na mipango ya Taasisi kama TBA kwa kuwa na miradi mingi zaidi ya ujenzi ili kuongeza makusanyo ya ndani na kupunguza utegemezi wa ruzuku kutoka Serikalini.
Awali akitoa taarifa za utekelezaji wa miradi hio, Mtendaji Mkuu wa TBA Arch. Daud Kandoro amesemakatika mwaka wa fedha 2022/23 tayari Serikali imeshatoa fedha kiasi cha shilingi bilioni 5.68 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la makazi ya watumishi wa umma katika eneo la Magomeni Kota awamu ya pili pamoja na kutoa fedha kiasi cha shilingi bilioni 4.3 kwa ajili ya kuendelea na uendelezaji wa eneo la Temeke Kota awamu ya kwanza.
Arch. Kondoro amesema TBA inaendelea kutekeleza miradi mingine nchi nzima kwa fedha za ruzuku na makusanyo ya ndani ikiwa na lengo la kutatua changamoto ya makazi kwa Watumishi wa Umma.