Mkuu wa mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amefanya ziara ya kutembelea Mradi wa ujenzi wa Mji wa Serikali unaotekelezwa katika eneo la Mtumba Jijini Dodoma.
Kupitia ziara hiyo, RC Senyamule amesema mkoa wa Dodoma umepata fursa ya kuwa na Mji wa Serikali ambao ni sehemu ya kivutio kwa watu ambao wanakuja mkoani Dodoma hivyo utaongeza utalii na kukuza uchumi.
Akikagua Jengo la Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na utawala bora ambalo limefikia zaidi ya asilimia 95 za utekelezaji, RC Senyamule amesema,
"Jengo hili limefikia hatua za mwisho hivyo ni muhimu Wakandarasi kuhakikisha wanakamilisha kwa wakati, nimeona miundombinu ya kisasa sambamba na upandaji wa miti ambayo inapendezesha eneo hili, pia nimeona barabara za lami zinazounganisha eneo hili la mradi".
Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Juma Mkomi amemtaka Mkandarasi wa jengo hilo ambaye ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) na Mshauri Elekezi Watumishi Housing kuhakikisha wanakamilisha mradi katika kipindi husika ili kuendana na maelekezo ya Serikali.
Naye, Kaimu Meneja Sehemu ya Ujenzi kutoka TBA Mhandisi Manase Shekalaghe amesema wamejipanga kukamilisha mradi huo kwa wakati ambapo hadi sasa kazi zinafanyika usiku na mchana ili kuendana na maelekezo yaliyotolewa na Serikali