Wanafunzi 13 wa kozi ya Ubunifu Majengo (Architecture), kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) wametembelea Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kwa lengo la kujifunza na kuona miradi inayotekelezwa na TBA katika mkoa wa Dodoma.
Wanafunzi hao, wanaosoma mwaka wa nne, wameweza kuona ofisi za wizara mbalimbali zinazojengwa katika mji wa Serikali eneo la Mtumba na kuvutiwa usanifu na mpangilio wake. Akiongea katika ziara hiyo, Meneja wa TBA mkoa wa Dodoma, Qs. Emmanuel Wambura, amesema miradi yote inayotekelezwa na TBA inazingatia ubora na usalama kwa watumiaji.
"Kabla ya kuanza ujenzi wa mji wa serikali, tulishirikiana na taasisi nyingine kufanya utafiti katika eneo lote la mji huu na kubaini sehemu za kujenga majengo hayo ambayo yamezingatia usalama kwa watumiaji" amesisitiza Qs. Wambura.
Nao wanafunzi Dorina Ngonde, Lusungu Mgole na Prisilla Kiagi kwa niaba ya wenzao, wameeza kuvutiwa na miradi ya TBA kuanzia kwenye usanifu na hata ujenzi wake. Wamebainisha kuwa majengo na miundombinu mingine ya mji wa serikali imeakisi ubunifu mzuri uliofanyika. Pamoja na kutembelea mji wa serikali pia walipata kujifunza kuhusu historia ya TBA na kazi zake ukiwepo mradi wa ujenzi wa nyumba 3500 za makazi ya watumishi wa umma unaotekelezwa katika eneo la Nzuguni.
Naye Arch. Sylivia Munisi, mwalimu aliyeambatana na wanafunzi hao, ameshukuru uongozi wa TBA kwa kuwapokea na kuwapa ushirikiano wa kutosha hali iliyopelekea kufahamu shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA).